Ajifungua mapacha 5 baada ya miaka 12 ya kusubiri mtoto
Eric Buyanza
May 8, 2026
Share :

Mwanamke mmoja nchini Ethiopia amejifungua watoto watano mapacha katika tukio la nadra baada ya kusubiri kupata mtoto kwa miaka 12, katika Jimbo la Harari.
Taarifa za hospitali ya Hiwot Fana, imesema Bedriya Adem, mwenye umri wa miaka 35, alijifungua watoto wa kiume wanne na wa kike mmoja, wote wakiwa wako katika hali nzuri ya afya.
Akizungumza na BBC, Bedriya alisema yeye na mumewe wamefurahia sana “kubarikiwa watoto watano kwa pamoja” baada ya miaka mingi ya maumivu ya kihisia na kuzongwa na jamii kutokana na kuchelewa kupata mtoto.
“Siwezi kueleza furaha yangu kwa maneno. Nilikuwa nikisubiri (mtoto) kwa maumivu makubwa hadi ndoto yangu ilipotimia,” alisema.
Daktari mkuu wa hospitali hiyo, Dkt Mohammed Nur Abdulahi, alisema mama na watoto wanaendelea vizuri chini ya uangalizi wa madaktari. Watoto hao walizaliwa kwa njia ya upasuaji na walikuwa na uzito wa kati ya kilo 1.3 na 1.4.
Hospitali hiyo ilisema ujauzito huo ulitungwa kawaida bila kutumia teknolojia ya upandikizaji ya IVF, jambo linalofanya tukio hilo kuwa la nadra zaidi, kwani uwezekano wa kupata mapacha (idadi hiyo) kwa njia ya asili ni mmoja kati ya milioni 55.
Bedriya alisema awali alielezwa kuwa alikuwa na watoto wanne tumboni, lakini alishangaa kujifungua mtoto wa tano.
“Nilikuwa nikiomba mtoto mmoja tu, lakini Mwenyezi Mungu amenipa watano,” alisema.
Watoto hao wamepewa majina ya Naif, Ammar, Munzir, Nazira na Ansar.





