Kane atupia tena wakati bayern ikitinga fainali ya DFB Pokal
Eric Buyanza
April 23, 2026
Share :

Bayern Munich imepiga hatua kuelekea kushinda mataji matatu, kwa kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho la Ujerumani – DFB Pokal kwa mara ya kwanza tangu 2020. Bayern waliwatandika Bayer Leverkusen 2 – 0 Jumatano usiku.
Mfungaji bora Harry Kane alifunga tena, siku tatu baada ya Bayern kutetea taji lao la Bundesliga na siku ambayo timu yao ya wanawake pia ilitwaa ubingwa. Luis Díaz alifunga la pili katika dakika za mwisho za mchezo.
Leverkusen iliiondoa Bayern katika raundi ya 16 msimu uliopita, lakini mara hii hawakuwa katika ubora wao.
"Ni siku maalum kwa klabu nzima na tunafurahi kuwa katika fainali," nahodha wa Bayern Manuel Neuer aliambia televisheni ya ZDF. “Tunapaswa kuangazia michezo ijayo.”
Mabingwa wa Kombe hilo VfB Stuttgart watawakaribisha wapinzani wao wa kusini-magharibi Freiburg katika nusu fainali ya pili Alhamisi, huku fainali ikifanyika Berlin Mei 23.
Nahodha wa Leverkusen, Robert Andrich, ambaye timu yake iko nje ya nafasi za Ligi ya Mabingwa katika Bundesliga, alisema: "Tumesikitishwa sana kwani ilikuwa nafasi kubwa ya kufika Berlin tena. "Katika dakika 90, ushindi wao ulistahili."
Bayern watakuwa na mchezo wa kwanza wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa dhidi ya mabingwa watetezi Paris Saint-Germain Jumanne ijayo huku wakilenga kushinda mataji matatu na pengine mataji sita kama mwaka 2020, walipowashinda Leverkusen katika fainali ya Kombe la DFB.
Kocha wa Bayern Vincent Kompany alisema: "Jambo gumu kuhusu mpira wa miguu ni kwamba huwezi kufurahia ushindi kikamilifu. Unasonga mbele kwenye mchezo mwingine muhimu."





