Kanisa lamsimamisha Padri anayetuhuiwa mauaji ya Asimwe
Sisti Herman
June 21, 2024
Share :
Kanisa Katoliki Jimbo la Bukoba limemsimamisha kutoa huduma za kichungaji Padri, Elipidius Rwegoshora kufuatia tuhuma zinazomkabili za kuhusika katika mauaji ya mtoto mwenye ulemavu wa ngozi, Asimwe Novart.
Askofu wa Jimbo Katoliki Bukoba, Jovitus Mwijage ametangaza uamuzi huo kupitia gazeti la Kiongozi linalotolewa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), toleo lake la Juni 21 -27, 2024
Gazeti hilo limemnukuu Askofu Mwijage akikiri kuwa mtuhumiwa ni padri wa jimbo lake na amemsimamisha kutoa huduma zote za kichungaji mpaka hapo suala lake litakaposhughulikiwa na vyombo vya sheria.
“Tunahuzunishwa na taarifa ya mauaji ya Asimwe, kwani sisi kama Kanisa Katoliki ni walinzi wa kwanza wa uhai wa wanadamu. Tunaiombea familia yake na kuiombea roho yake ipate pumzio la amani mbinguni.
“Hata hivyo, tumesikia taarifa ya watuhumiwa na mmojawapo akiwa ni Padri Rwegoshora. Ni kweli padri huyo ni wa jimbo Katoliki Bukoba na tumechua uamuazi wa kumsimamisha kutoa huduma zote za kichugaji mpaka hapo suala lake litakaposhughulikiwa na vyombo vya sheria.
“Baada ya vyombo vya sheria kumaliza kazi yake, ndipo taratibu nyingine za kanisa zitafuata,” amesema Askofu Mwijage.
Asimwe menye umri wa miaka miwili na nusu alinyakuliwa mikononi mwa mama yake na watu wasiojulikana Mei 30, 2024 katika Kijiji cha Bulamula, Muleba mkoani Kagera.