Kuachia watoto mitandao ya kijamii ni kutengeneza bomu
Eric Buyanza
July 27, 2026
Share :

Imeelezwa na wataalam kuwa kuwaacha watoto kutumia majukwaa ya mitandao ya kijamii bila uangalizi ni kutengeneza ‘bomu’ ambalo baadaye litakuwa vigumu kulidhibiti.
-
Mwito huo umetolewa wakati wataalamu wakisisitiza umuhimu wa kuongeza elimu kwa wazazi, walezi na watoto kuhusu matumizi salama ya mitandao, huku mataifa mbalimbali yakiendelea kuimarisha sheria za kuwalinda watoto dhidi ya madhara ya matumizi ya majukwaa ya kidijitali.
-
Mwito huo unakuja wakati Ufaransa imepitisha sheria ya kupiga marufuku watoto walio chini ya umri wa miaka 15 kutumia mitandao ya kijamii ikiwa ni nchi ya pili baada ya Australia, ambayo tayari imeweka marufuku kwa watoto walio chini ya miaka 16, huku mataifa mengine yakijadili sheria kama hizo ili kuimarisha ulinzi wa watoto mtandaoni.
-
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge na mtaalamu wa saikolojia, Dk Peter Siamoo alisema watoto wanapoachwa kutumia mitandao bila mwongozo hukutana na maudhui ambayo hawana uwezo wa kuyachuja, jambo linaloweza kuathiri maadili, afya ya akili na mwenendo wao.
-
“Hii mitandao tukiifanya ndiyo mlezi wa watoto wetu, baadaye itakuwa bomu kubwa. Wazazi wanapaswa kuwa makini na kuhakikisha wanajua watoto wao wanaangalia nini na kwa muda gani,” alisema Dk Siamoo ambaye pia ni Padri wa Kanisa Katoliki.
-
Alisema kuzuia matumizi ya simu pekee kwa watoto haitoshi sababu kuna komputa pia ambazo hutumika kujifunza shuleni na wanafunzi wakati mwingine hutumia kutizama mambo yasiyofaa.
Source: HabariLeo





