Marekani yamsaka rubani wake baada ya ndege kudunguliwa
Eric Buyanza
April 4, 2026
Share :

Ripoti zinaonyesha kuwa Marekani na Iran zinashindana kwa kasi kumtafuta rubani wa pili wa ndege ya kivita ya Marekani iliyodunguliwa katika eneo la kusini mwa Iran.
Operesheni hiyo imekuwa ya dharura huku pande zote zikijaribu kumfikia rubani huyo kabla ya mwingine. Hapo awali, uchunguzi wa BBC Verify ulithibitisha video iliyokuwa ikisambaa mtandaoni ikionyesha kile kinachoonekana kuwa ndege ya Marekani ikifuatana na helikopta mbili, zikifanya operesheni ya utafutaji na uokoaji.
Video hiyo ilithibitishwa kushambuliwa katika jimbo la Khuzestan, karibu na daraja juu ya mto Karun.Video hiyo imechunguzwa ili kuthibitisha kuwa ni ya hivi karibuni na pia kuangaliwa kama ina dalili zozote za kutengenezwa kwa teknolojia ya AI, lakini hakuna ushahidi uliopatikana unaoonyesha udanganyifu.
Hii inaongeza uzito wa taarifa kuwa operesheni hiyo ni halisi.
Kwa mujibu wa ripoti kutoka Marekani, zikimnukuu maafisa wasiotambulishwa majina, operesheni hiyo imefanikiwa kumwokoa mmoja wa wahudumu wa ndege hiyo, lakini juhudi bado zinaendelea kumtafuta rubani wa pili ambaye hajapatikana. Wataalamu wa masuala ya kijeshi wanaeleza kuwa operesheni kama hizi ni hatari sana na zinahitaji kufanyika kwa haraka zaidi.
James Jeffrey, mwanadiplomasia wa zamani wa Marekani, amesema kuwa hii ni miongoni mwa oparesheni hatari zaidi za kijeshi, kwani hujumuisha helikopta, ndege za kuongeza mafuta angani, na ndege za kulinda eneo hilo. Kwa upande mwingine, mhudumu na rubani wa ndege walioanguka huwa wamefunzwa kukabiliana na hali kama hizi.
Kipaumbele chao kikuu ni kubaki hai na kuepuka kukamatwa, ikiwa ni pamoja na kujificha na kuondoka haraka katika eneo walipoangukia.
Aidha, hupatiwa mafunzo ya mbinu za kuishi mazingira magumu, ikiwa ni pamoja na jinsi ya kupata chakula na maji au kuhimili bila hivyo kwa muda.
Hii huwasaidia kuongeza nafasi ya kuokolewa kabla hawajapatikana na maadui.
BBC





