TFF yapigwa faini ya mamilioni kisa Kocha
Sisti Herman
January 22, 2024
Share :
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetozwa faini ya Sh25 milioni kutokana na uvunjaji wa maadili uliofanywa na kocha wa timu ya Taifa ya Tanzania, Adel Amrouche hivi karibuni, uliosababisha kocha huyo apewe adhabu ya kufungiwa mechi nane.
Adhabu hiyo imetolewa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kwa kile kilichodaiwa kuwa ni uchochezi kuwa Morocco ina ushawishi ndani ya CAF katika kupanga mechi pamoja na waamuzi.
TFF imetozwa faini kutokana na kuvunja kanuni ya 110 ya fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) inayotaka timu shiriki kudhibiti mwenendo wa ofisa/maofisa wake.
“Chama shiriki kinapaswa kuwajibika kwa tabia za wahusika wa msafara wake (maofisa na wachezaji) katika kipindi chote hadi mwisho wa shindano,” inafafanua kanuni hiyo.