Ukraine kupewa leseni ya kutengeneza makombora ya Patriot
Eric Buyanza
July 9, 2026
Share :

Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema yuko tayari kuipa Ukraine leseni ya kutengeneza makombora ya kujihami ya Patriot, hatua ambayo inaweza kusaidia nchi hiyo kuimarisha ulinzi dhidi ya mashambulizi ya makombora ya masafa marefu kutoka Urusi.
Akizungumza na Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelensky, wakati wa mkutano wa NATO uliofanyika Ankara Jumatano, Trump alisema: "Tutawapa leseni ya kutengeneza Patriot. Nafikiri wanaweza kuanza kuzalisha kwa haraka mara tu tutakapowapa maelekezo."
Trump alisema bado hajawafahamisha watengenezaji wa mifumo hiyo ya ulinzi, kampuni za Lockheed Martin na Raytheon, kuhusu uamuzi huo, lakini aliongeza kuwa anaamini suala hilo litashughulikiwa vizuri.
Mfumo wa Patriot hutambua na kuharibu makombora yanayolengwa angani na unachukuliwa kuwa miongoni mwa mifumo bora zaidi ya ulinzi wa anga duniani.
Hata hivyo, pia ni miongoni mwa mifumo ghali zaidi, ambapo betri moja kamili yenye makombora yake hugharimu takriban dola bilioni moja za Marekani.
Aidha, uzalishaji wake huchukua muda mrefu, huku takribani makombora 600 pekee yakizalishwa kwa mwaka, kwa mujibu wa Idara ya Ulinzi ya Marekani.
Marekani imekuwa na tahadhari kuhusu kutoa mifumo hiyo kutokana na kuwa ilitumia zaidi ya nusu ya akiba yake ya makombora ya Patriot wakati wa vita vyake na Iran mapema mwaka huu, kwa mujibu wa taasisi ya utafiti ya Center for Strategic and International Studies (CSIS).
"Tunayo mifumo ya Patriot, lakini si mingi. Tunaihitaji pia kwa ajili ya kujilinda sisi wenyewe," alisema Trump.
Hata hivyo, Ukraine inahitaji kwa dharura mifumo ya ulinzi ya Patriot ili kujikinga dhidi ya mashambulizi ya Urusi.
Katika miezi ya hivi karibuni, Moscow imeongeza mashambulizi ya makombora ya masafa marefu dhidi ya Ukraine, na kusababisha vifo vya watu kadhaa, hususan katika mji mkuu, Kyiv.
Katika kipindi cha wiki iliyopita pekee, mashambulizi hayo yamesababisha vifo vya makumi ya watu mjini humo.
BBC





