Vita yaanza upya baada ya Iran kudungua helikopta ya Marekani
Eric Buyanza
June 10, 2026
Share :

Marekani na Iran zimeshambuliana baada ya Marekani kutishia kulipiza kisasi kufuatia kudunguliwa kwa helikopta ya kijeshi ya Marekani juu ya Mlango wa Hormuz siku ya Jumatatu.
Jeshi la Marekani lilisema Jumanne kuwa limekamilisha mashambulizi ya anga yaliyoanza saa 17:00 kwa saa za Marekani Mashariki.
Kwa upande wake, Jeshi la Mapinduzi la Iran (IRGC) lilisema lilifanya shambulio la ndege zisizo na rubani dhidi ya kambi ya Marekani nchini Bahrain na shambulio la makombora dhidi ya kambi ya Marekani nchini Jordan, huku jeshi la Kuwait likiripoti kuwa lilikuwa likizuia mashambulizi.
Marekani imesema mashambulizi yake ni “jibu” kwa kudunguliwa kwa helikopta hiyo, tukio ambalo Rais Donald Trump alilitaja kuwa lilifanywa na Iran, wakati IRGC likiyaita mashambulizi ya Marekani kuwa “ya kikatili”.
Tukio hilo lilitokea baada ya wafanyakazi wawili wa helikopta ya Marekani ya Apache kuokolewa na droni ya majini ya Marekani siku ya Jumatatu, ikiwa ni mara ya kwanza kwa jeshi la Marekani kutumia aina hiyo ya chombo katika operesheni ya uokoaji.
Maafisa wa Marekani walisema Iran ilitumia droni kushambulia helikopta hiyo, lakini bado haijathibitishwa kama shambulio hilo lilikuwa la makusudi. Shirika la habari la Mehr liliripoti kuwa Iran haijakiri kuhusika.
Centcom ilisema ndege za kivita za Marekani zilishambulia mifumo ya ulinzi wa anga ya Iran, vituo vya udhibiti wa ardhini, na rada karibu na Mlango wa Hormuz.
Kwa upande mwingine, IRGC ilisema mashambulizi ya Marekani yameharibu mnara wa mawasiliano na matenki mawili ya maji.
BBC





