"Wakati wangu umefika mwisho", Elon Musk aondoka Ikulu
Eric Buyanza
May 29, 2025
Share :
Elon Musk, bilionea na mmiliki wa X (zamani Twitter), amethibitisha kuondoka kwenye serikali ya Rais Donald Trump.
Musk alikuwa akiongoza juhudi kubwa za kupunguza matumizi ya serikali ya Marekani, zilizosababisha maelfu ya nafasi za kazi za serikalini kufutwa.
Katika chapisho lake kwenye X, Musk alimshukuru Trump kwa fursa ya kusaidia kuendesha Idara ya Ufanisi Serikalini, inayojulikana kama DOGE.
Ikulu ya White House ilianza "kumuondolea" Musk nafasi yake kama mfanyakazi maalum wa serikali Jumatano usiku.
Jukumu lake lilikuwa la muda mfupi na kuondoka kwake hakukutarajiwa, lakini linakuja siku moja baada ya Musk kukosoa muswada wa bajeti ya Trump, ambao unapendekeza kusitishwa kwa kodi ya mamilioni ya dola na ongezeko la matumizi ya ulinzi.
Musk alieleza kuwa muda wake kama mfanyakazi maalum wa serikali umefikia kikomo, na akaeleza shukrani zake kwa Rais Trump kwa fursa ya kupunguza matumizi mabaya.
Alisisitiza kuwa "DOGE itaendelea kuimarika kadiri inavyokuwa sehemu ya maisha katika serikali," akionyesha imani yake katika kuendelea kwa mradi huo.
Kulingana na makadirio, takriban wafanyakazi 260,000 kati ya milioni 2.3 wamepoteza kazi zao kutokana na mradi huo wa DOGE.