Wananchi wajitokeza kung'oa visiki vya mirungi
Eric Buyanza
June 2, 2025
Share :
Katika jitihada za kuimarisha mapambano dhidi ya dawa za kulevya nchini, wananchi wa Kijiji cha Heikonti kilichopo Kata ya Tae, Wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro, wamejitokeza kwa hiari kung’oa visiki vya mirungi zao haramu linalotumika kama dawa ya kulevya ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa operesheni ya kuondoa kabisa kilimo cha mirungi katika eneo hilo.
Ofisa Elimu Kanda ya Kaskazini wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Shaban Miraji, ambaye alithibitisha kuwa zoezi hilo limefanyika kwa mafanikio makubwa kwa kushirikiana na Serikali ya Wilaya ya Same pamoja na wananchi wenyewe.
"Ni hatua ya kihistoria kuona wananchi wa Heikonti wakijitokeza kwa hiari kung’oa visiki vya mirungi, jambo linalothibitisha kwamba elimu dhidi ya kilimo cha dawa za kulevya inaendelea kuzaa matunda chanya," amesema Miraji.
Miraji anasema hamasa hii ya wananchi imechangiwa kwa kiasi kikubwa na elimu iliyotolewa na mamlaka mbalimbali za Serikali, ikiwemo DCEA yenyewe, kuhusu madhara ya mirungi na faida ya kuachana na kilimo hicho. Serikali imekwishaandaa mbadala wa mazao zaidi ya nane kwa ajili ya wanakijiji wa Kata ya Tae, Vudee na maeneo mengine yaliyokuwa na historia ya kilimo cha mirungi.
Zoezi hili la kung’oa visiki linatokana na operesheni kubwa ya kitaifa ya uteketezaji wa mashamba ya mirungi iliyofanyika mwezi Machi 2025, chini ya usimamizi wa Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas James Lyimo, katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Same.
NIPASHE