Zaidi ya viwanda 100 vya pombe vyafungwa kulinda afya za wananchi
Eric Buyanza
August 7, 2026
Share :

Rwanda imeanzisha kampeni kali ya kitaifa dhidi ya pombe zisizo salama na zisizokidhi viwango, baada ya mamlaka kuripoti vifo vya zaidi ya watu 50 na mamia ya wengine kuugua kutokana na vinywaji hivyo.
Serikali inasema operesheni hiyo inalenga kuondoa sokoni pombe hatari, kuwachukulia hatua wazalishaji wanaokiuka sheria na kupunguza madhara ya kiafya na kijamii yanayotokana na matumizi mabaya ya pombe.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya, baadhi ya vinywaji vilivyokaguliwa vimekutwa na kemikali hatari, ikiwemo methanoli. Kemikali hiyo inaweza kusababisha madhara makubwa, yakiwemo kupoteza uwezo wa kuona, kuharibika kwa viungo vya mwili na hata kifo.
Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Rwanda pamoja na Shirika la Taifa la Viwango zimechukua hatua dhidi ya wazalishaji wanaodaiwa kukiuka masharti ya usalama. Zaidi ya viwanda 100 vimefungwa, watu kadhaa kukamatwa, leseni kufutwa na bidhaa kadhaa kuondolewa sokoni.
Wasambazaji na wafanyabiashara pia wameagizwa kuacha kuuza vinywaji vilivyopigwa marufuku na kuviondoa katika maeneo yao ya biashara.





