ZELENSKY ALEGEZA KAMBA? Tuko tayari kusitisha mashambulizi dhidi ya Urusi
Eric Buyanza
September 16, 2026
Share :

Rais Volodymyr Zelensky amesema Ukraine iko tayari kusitisha mashambulizi yake ndani ya eneo la Urusi endapo washirika wataweza kupata ahadi ya kweli kutoka kwa Urusi ya kutoishambulia miundombinu muhimu ya Ukraine.
Kauli hii inajiri wakati shambulio la droni la Urusi limesababisha kukatika kwa umeme katika baadhi ya maeneo ya mji wa Zaporizhzhia na kumuua mtu mmoja, huku wasiwasi kuhusu usalama wa nishati ukiongezeka.
Wakati majibizano ya kidiplomasia yakiendelea, Rais wa Marekani Donald Trump amesema kwamba Urusi na Ukraine wamekubaliana kuepuka kushambulia miundombinu ya nishati ya kila mmoja, ingawa hakutoa maelezo ya kina kuhusu makubaliano hayo. Kupitia mtandao wake wa Truth Social, Trump amedai kupanda kwa bei ya dizeli duniani kunasababishwa zaidi na vita ya Urusi na Ukraine kuliko mgogoro wa Iran.
Zelensky amesema hatua ya kupunguza mashambulizi dhidi ya miundombinu muhimu inaweza kuwa "hatua ya kwanza kuelekea amani,” lakini akasisitiza kwamba Kyiv iko tayari endapo kutakuwa na dhamana ya dhati kutoka Moscow.
"Endapo washirika wetu wa Marekani watafanikiwa kuhakikisha utayari wa kweli wa Urusi kusitisha vita hivi, na kufanya hivyo kwa uaminifu na kwa muda mrefu, basi Ukraine itachukua hatua zake za kupunguza mvutano. Amani inahitajika. Masuala ya nishati, njia za usambazaji chakula, na miundombinu muhimu yote yanapaswa kujadiliwa katika mazungumzo ya kusitisha mashambulizi. Uamuzi thabiti na wa haki unahitajika — si kwa ajili ya uchaguzi, bali kwa muda wote. Tunawasubiri washirika wetu watoe maelezo mahsusi.”
Ameongeza kusema kwamba Urusi imekuwa ikivilenga hasa vituo vya nishati, bandari, maghala ya chakula na dawa, na kwamba Ukraine haijashawishika kama Moscow iko tayari kuheshimu makubaliano yoyote.
Huku majadiliano hayo yakiendelea, mashambulizi mapya yameripotiwa. Droni ya Urusi ilikilenga kituo cha mafuta mjini Kyiv, ikimjeruhi mtu mmoja, na mashambulizi mengine yakalenga maghala ya bidhaa.
Mamlaka za Ukraine zinasema Urusi imeshambulia takriban vituo 300 vya mafuta katika miezi ya hivi karibuni, hasa karibu na eneo la mapambano.
Ndani ya Urusi, mashambulizi ya Ukraine yameendelea. Kombora la Ukraine liliharibu ghala la kampuni ya Ozon katika mji wa bandari wa Taganrog, huku shambulio la droni likilenga kiwanda katika mkoa wa Samara, eneo lenye mitambo mikubwa ya kusafishia mafuta.





